RAIS SAMIA AHIMIZA USHIRIKIANO KUINUA TASNIA YA KAHAWA AFRIKA
- Aahidi kuongeza bajeti ya kuendeleza sekta kilimo nchini
- Serikali kuongeza jitihada za kuongeza wigo wa soko la kahawa nje ya nchi
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa rai kwa nchi za Afrika zinazozalisha kahawa kushirikiana ili kukuza soko la kahawa na kufungua fursa za ajira kwa vijana na wanawake barani Afrika.
Rais Samia ametoa rai hiyo alipozungumza katika Mkutano wa Tatu wa G25 wa Wakuu wa Nchi za Afrika zinazozalisha Kahawa uliofanyika jijini Dar es salaam katika ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere
Rais Samia amesisitiza umuhimu wa nchi za Afrika kununua kahawa ya Afrika baada ya kuwa imeongezewa thamani kwa lengo la kukuza biashara ya kahawa miongoni mwa nchi za Afrika na hivyo kuimarisha sekta ya kahawa barani Afrika.
Mkutano huo, ulioendeshwa chini ya kaulimbiu isemayo "Kufungua Fursa za Ajira kwa Vijana Kupitia Uendelezaji wa Sekta ya Kahawa Afrika" uliwaleta pamoja viongozi kutoka nchi 25 za Afrika zinazozalisha kahawa, wataalamu wa sekta ya kahawa na wawekezaji ili kujadili njia za kufufua sekta ya kahawa barani Afrika.
Rais Samia amesisitiza dhamira ya Tanzania ya kuongeza uzalishaji wa kahawa, kukuza biashara ya kahawa, kuongeza mnyororo wa thamani wa zao la kahawa na hivyo kukidhi mahitaji ya soko.
Amesisitiza pia umuhimu wa kutokusafirisha kusafirisha kahawa ghafi na kuwekeza katika viwanda vya usindikaji wa ndani ili kuongeza mapato na kutoa ajira kwa vijana wa Tanzania. "Lazima tukubaliane hapa, kahawa inayozalishwa Afrika inapaswa kusindikwa hapa hapa Afrika na kisha iuzwe nje ya bara hili, kuendelea kusafirisha kahawa ghafi ni kuuza ajira ya vijana wa Afrika nje ya bara, kuua soko la Kahawa na kuua mioyo ya wakulima kwani hawaoni manufaa ya kazi zao," alisema.
"Afrika inazalisha baadhi ya kahawa bora zaidi duniani, lakini bado tunabaki kuwa wauzaji wakuu wa Kahawa ghafi. Tunapaswa kubadilisha hali hii kwa kuhakikisha kahawa inayozalishwa Afrika inaongezwa thamani hapa hapa katika bara la Afrika, na kuimarisha biashara ya kikanda, na ndipo iuzwe nje ya bara la Afrika"amesisitiza Rais Samia.
Rais Samia pia ameeleza kuwa ushirikishwaji wa vijana katika sekta ya kahawa ni muhimu ili kuendeleza sekta hiyo na alizihimiza nchi za Afrika na wadau wa sekta hiyo kuwekeza katika programu za mafunzo, kutoa pembejeo za kilimo kwa wakulima kwa kuwapa miche ya kahawa, mbolea na dawa za kuua wadudu pamoja na mbinu za kilimo za kisasa ili kuvutia vijana katika kilimo cha kahawa na usindikaji.
Rais Samia amesema kuna haja ya kuifanya Afrika kuwa soko kubwa la kahawa kwa kuhakikisha Kahawa inalimwa kwa wingi na kusindikwa barani Afrika.
Amesema Tanzania itaenda kutafuta soko la Kahawa iliyosindikwa ya Tanzania kwa mataifa mengine kama ya kutoka Mashariki ya Kati ambao alisema ni miongoni mwa watumiaji wakubwa wa kahawa duniani.
Alizisihi nchi za Afrika kukukubaliana kupitia Azimio la Dar es Salaam kuhusu Kahwa ambalo alisema kuwa linapaswa kuonyesha njia watakayoitumia nchi za Afrika ili kuwa soko kubwa la kahawa Duniani na jinsi watakavyofikia hatua hiyo na kuongeza kuwa uwepo wa soko la uhakika ndio jambo lka msingi.
Amesema Tanzania inalenga kuongeza uzalishaji na ubora wa kahawa ili kukidhi mahitaji ya soko la kimataifa, kwa kuwawezesha vijana kushiriki katika kilimo kwa kuwapa miche na ruzuku ya mbolea. Aliongeza kuwa kwa kufanya hivyo tutakuza soko la kahawa na kuvutia vijana.